KOCHA Mkuu wa Songea United ya Songea, mkoani Ruvuma, Juma Masoud amesema anahitaji muda zaidi kwa ajili ya kutengeneza timu ya ushindani, licha ya kutojua hatima yake kwa sasa baada ya mkataba wake kumalizika mwisho wa msimu wa 2025-2026.
Akizungumza na Soka la Bongo, Masoud aliyewahi kuifundisha FGA Talents kwa sasa Fountain Gate, amesema licha ya kuichukua timu hiyo katikati ya msimu ila kumekuwa na mabadiliko chanya ya kiuchezaji kwa wachezaji, tofauti na matarajio yake.
“Kumekuwa na mabadiliko chanya ya kiuchezaji jambo ambalo benchi la ufundi tunajivunia maendeleo ya kila mmoja wao, hii ni kutokana na mradi mzuri wa wenzangu waliouacha, kitu ambacho kimechangiwa na ushirikiano wetu sote,” amesema Masoud.
Masoud aliyejiunga na kikosi hicho Januari 2026, akichukua nafasi ya Meja Mstaafu, Abdul Mingange aliyeanza nayo msimu wa 2025-2026, kwa sasa timu hiyo imeshinda mechi saba, sare nane na kupoteza tisa, ikishika nafasi ya nane na pointi 29.
Msimu wa 2024-2025, Masoud akiifundisha Stand United, aliiongoza kumaliza nafasi ya tatu katika Ligi ya Championship na pointi 61, jambo lililoiwezesha kucheza mechi za ‘Play-Off’ za kusaka tiketi ya kupanda Ligi Kuu Bara, ingawa, alikwama.
Stand United iliyoshuka daraja kutoka Ligi Kuu msimu wa 2018-2019, ilianza kucheza ‘Play-Off’ ya kwanza kwa kishindo kwa kuiondosha Geita Gold kwa jumla ya mabao 4-2, baada ya kikosi hicho cha mjini Geita kumaliza nafasi ya nne na pointi 56.
Baada ya Stand kuitoa Geita Gold, ikacheza ‘Play-Off’ nyingine na Fountain Gate iliyotolewa pia hatua hiyo na maafande wa Tanzania Prisons kwa jumla ya mabao 4-2, ambapo kikosi hicho kilikwama kupanda baada ya kufungwa jumla ya mabao 5-1.
The post MASOUD AOMBA MUDA SONGEA UNITED appeared first on Soka La Bongo.
from Soka La Bongo https://ift.tt/uVWs3Od
via IFTTT
Post a Comment