KOCHA Mkuu wa Yanga SC, Pedro Goncalves, amesema akili na nguvu zote za kikosi chake zimeelekezwa katika kusaka pointi muhimu kwenye mchezo wa marudiano wa hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya AS FAR Rabat
Pedro amesema kuwa matokeo ya mchezo huo yataamua hatma ya timu hiyo kucheza hatua ya robo fainali.
Kikosi cha Yanga kimesafiri jana kuelekea nchini Morocco kwa ajili ya mchezo huo unaotarajiwa kuchezwa Februari 7, 2026, ambapo kocha huyo ameeleza kuwa wanauchukulia kama fainali kutokana na uzito wake katika msimamo wa kundi.
Pedro amesema katika mchezo huo hawapaswi kuruhusu kufungwa zaidi ya bao moja, huku lengo lao kubwa likiwa ni kupambana kusaka ushindi au angalau pointi moja ili kuendelea kuweka hai matumaini ya kufuzu.
“Endapo tutapoteza kwa tofauti ya bao 1-0 bado tunaweka matumaini yetu hai, lakini tukifungwa zaidi ya hapo tutakuwa tumeaga mashindano na kusubiri msimu ujao,” amesema Pedro.
Ameongeza kuwa sare haitakuwa matokeo mabaya kwao kwani itaendelea kuwaweka kwenye mchakato wa kufuzu, huku ushindi ukiwa ni tiketi ya moja kwa moja ya kusonga mbele hadi hatua ya robo fainali wakiwa ugenini nchini Morocco.
Pedro amesisitiza kuwa ni mechi muhimu sana kwa Yanga, na kikosi chake kinaenda kupambana kwa nguvu zote kusaka matokeo chanya yatakayowafikisha katika malengo yao ya msimu huu wa Ligi ya Mabingwa Afrika.
The post YANGA KUSAKA POINTI MOROCCO appeared first on Soka La Bongo.
from Soka La Bongo https://ift.tt/cJfAkH4
via IFTTT
Post a Comment