JINAMIZI la mwenendo mbovu wa matokeo limeendelea kuikumba KMC msimu huu, huku kocha wa kikosi hicho, Abdallah Mohamed ‘Baresi’, akiendeleza rekodi mbaya, tangu alipojiunga nayo Desemba 30, 2025, akichukua nafasi ya Marcio Maximo raia wa Brazil.
Februari 17, 2026, KMC FC ilitupwa nje ya michuano ya Kombe la Shirikisho (FA) kwa penalti 3-2 dhidi ya Bandari Tanzania ya Mtwara inayoshiriki First League (Ligi Daraja la Pili), baada ya timu hizo kutoka sare ya mabao 3-3, ikiwa ni mwenendo mbaya zaidi msimu huu.
Timu hiyo iliyotolewa hatua ya 64 bora ya michuano hiyo, Baresi ameiongoza mechi saba za mashindano yote tangu Desemba 30, 2025, ambapo sita ni za Ligi Kuu Bara na moja ya FA, akishinda moja na kutoka pia sare moja, huku akichapwa mitano na kuzidisha presha zaidi.
Akizungumza na Soka la Bongo, Baresi alisema walipoteza mechi hiyo kwa kukosa umakini kwa wachezaji wa timu hiyo, ingawa siyo muda wa kuanza kuangalia walipokosea kwa sababu imeshatokea, hivyo, wanaongeza nguvu katika kukinusuru kikosi hicho.
“Tulikuwa na uwezo wa kuimaliza mechi ndani ya dakika 90, ila bahati mbaya hatukufanya hivyo na wapinzani wetu wakatumia udhaifu huo, nadhani kwa sasa malengo yetu pekee ni kujirekebisha kwa mechi zijazo za Ligi Kuu Bara,” alisema Baresi.
Aidha, Baresi alisema kadri timu hiyo inavyozidi kupoteza mechi moja hadi nyingine ndivyo inavyoshusha morali ya nyota wa kikosi hicho, ingawa anaamini bado wana muda mzuri wa kuwajenga kisaikolojia na kurudisha matumaini waliyoyapoteza.
Baada ya KMC kutolea Kombe la Shirikisho (FA), nguvu kubwa ni kuinusuru timu hiyo isishuke daraja, kwa sababu hadi sasa ipo mkiani mwa Ligi Kuu ikikusanya pointi nane, baada ya kushinda mechi mbili, sare mbili na kupoteza 11, kati ya 15 ilizocheza.
The post REKODI ZA BARESI ZA ZASHTUA KMC appeared first on Soka La Bongo.
from Soka La Bongo https://ift.tt/oVBxAak
via IFTTT
Post a Comment