Simba, Yanga zilivyoiga utamaduni wa Ghana - EDUSPORTSTZ

Latest

Simba, Yanga zilivyoiga utamaduni wa Ghana



WAKATI naanza kuandika makala haya namkumbuka rafiki yangu kocha aliyewahi kufundisha timu kadhaa za taifa na klabu ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. Kocha huyu aliwahi kuniambia ni Tanzania pekee timu ya kigeni inapofungwa na mwenyeji wanaochukia na kuumia zaidi ni mashabiki wa Simba au Yanga kuliko hata timu zenyewe za kigeni.

Kisa kilianzia wapi?

Mwaka 1974, Simba iliwakilisha Tanzania katika Ligi ya Mabingwa Afrika (zamani Klabu Bingwa Afrika). Ilicheza dhidi ya Accra Hearts of Oak ya Ghana. Mchezo wa kwanza wa robo fainali ulichezwa ugenini. Simba ilifika hatua hiyo baada ya kuitoa Linare ya Maseru, Lesotho. Kabla ya mchezo dhidi ya Accra Hearts of Oak, mchezaji Willy Mwaijibe alikuwa amesimamishwa. Wachezaji wa Simba wakauomba uongozi arudishwe kutokana na umuhimu wa mchezo huo.

Uongozi ukakubali na jukumu hilo akapewa mchezaji Omary Gumbo kumfuata. Timu ikamaliza mazoezi Viwanja vya Gymkhana jijini Dar es Salaam na kuondoka nchini.

Asante Kotoko chanzo cha yote

Timu mbili za Ghana, Asante Kotoko na Accra Hearts of Oak zilikuwa na upinzani mkali mithili ya utani wa jadi wa Simba na Yanga. Simba ilipofika nchini humo, ikapokewa na Asante Kotoko na kuonyeshwa njia zote.


 
Lakini kwa bahati mbaya ikiwa katika maandalizi ya mchezo Mwaijibe akaumia mazoezini kiasi cha kutoweza kucheza.

Maandalizi yaliendelea viongozi wa Asante Kotoko wakawapa Simba mchongo mzima wa ndani na nje ya uwanja dhidi ya Accra Hearts of Oak. Simba waliambiwa wakati timu zinatoka vyumbani na kuingia uwanjani kuna mtoto mdogo atakatiza mbele ya msafara huo laiti kama wataweza kumdhibiti asikatize basi watashinda, vinginevyo watapokea kichapo.

Siku ya mechi viongozi wa Simba wakati wanatafakari na kujiuliza jinsi ya kulifanyia kazi ndipo Mwaijibe akawaambia yuko tayari kuifanya kazi ya kumdhibiti.

Mtoto adhibitiwa

Timu zikiwa zinatoka uwanjani Mwaijibe alimuona mtoto akitaka kupita mbele ya msafara.Alitoka kwa kasi na kumdhibiti. Yule mtoto alifurukuta kujiondoa maungoni mwa mchezaji huyo lakini hakufanikiwa. Mwaijibe alimwachia baada ya msafara wote kuingia uwanjani.

Kitendo hicho kilimfanya Mwaijibe asumbuliwe na polisi na mashabiki wa Accra Hearts of Oak wakiamini amewaharibia mipango yao ya nje ya uwanja.

Hadi mwisho Simba ilishinda 2-1 ugenini kwa mabao ya Abdallah ‘King’ Kibadeni na Adam Sabu. Mchezo wa marudiano Dar es Salaam uliisha kwa sare tasa na kufanikiwa kucheza nusu fainali dhidi ya Mehalla El Kubra ya Misri




Download our APP from Google Playstore using the link here>>>

Join Our Telegram Channel for Daily Updates CLICK HERE

No comments:

Post a Comment

Edusportstz