Watanzania Milioni Saba Wana Matatizo yanayohusiana na Afya ya Akili - EDUSPORTSTZ

Latest

Watanzania Milioni Saba Wana Matatizo yanayohusiana na Afya ya Akili




Wakati Dunia ikiadhimisha Siku ya Afya ya Akili kesho Jumapili Oktoba 10,2021, imeelezwa kuwa Tanzania inakadiriwa kuwa na watu milioni saba wenye matatizo yanayohusiana na afya ya akili.


Hata hivyo, sababu mbalimbali zimetajwa kusababisha matatizo ya afya ya akili huku Jiji la Dar es Salaam limetajwa kuwa na idadi kubwa ya wenye matatizo hayo.



Miongozi mwa sababu zilizotajwa kuchochea tatizo hilo ni msongo wa mawazo, ugumu wa maisha na matamanio ya kuwa na maisha bora.



Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa magonjwa yasiyoambukiza, Dk Shedrack Makubi amesema sababu ya Dar es Salaam kuwa na wagonjwa wengi ni kutokana na wingi wa watu katika jiji hilo ambalo lina mkusanyiko kutoka mikoa mbalimbali.



Pia, mazingira na harakati za kutafuta maisha kwa wakazi wa jiji hilo, zimetajwa kuwa kichocheo cha watu wengi kujikuta kwenye matatizo hayo ya kiafya.



Dk Makubi alitaja sababu nyingine ni matumaini ya watu mbalimbali kuwa Dar es Salaam kuna fursa nyingi za maisha na ajira hivyo, wanakuja kwa ajili ya kutafuta lakini, wanapofika mambo huwa tofauti na matarajio.



Alisema kuwa mambo yanapokuwa tofauti na matarajio, baadhi hujikuta kwenye wakati mgumu na kujiingiza kwenye makundi yasiyofaa likiwemo matumizi ya dawa za kulevya.



Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaonyesha kufikia mwaka 2020 watu bilioni moja walikuwa wanaishi na magonjwa ya akili huku wengi walio katika hatari ni wenye umri kuanzia miaka 15 hadi 39.



Mkurugenzi wa Hospitali ya Magonjwa ya afya ya akili ya Mirembe, Dk Paul Lawala alisema ugonjwa wa afya ya akili ni tatizo kubwa duniani kwani takwimu zinaonyesha watu milioni 300 duniani wanakabiliwa na tatizo la afya ya akili, ambapo wanahitaji msaada wa kisaikolojia na waliofikia viwango vya juu wanahitaji matibabu.



Undani magonjwa ya akili

Meneja wa Mpango wa Taifa wa Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa Yasiyoambukiza kutoka Wizara ya Afya, Dk Omary Ubuguyu, amesema kuna magonjwa zaidi ya 340 ya akili yaliyogawanywa katika makundi tofauti.



“Kwa kiasi kikubwa magonjwa ya akili yanahusishwa na kupotea kwa nguvukazi, kwa kuwa magonjwa haya yasipotibiwa kwa wakati, wagonjwa wengi hushindwa kurudi kwenye uwezo wao na hivyo, kuathiri uwezo wa uzalishaji.

&t;br />

Kwa jumla magonjwa ya akili yanachangia kwa zaidi ya asilimia 40 ya athari za kiafya kwa mtu mmoja mmoja na jamii,’’ amesema.



“Hii inamaanisha kuwa, jamii yetu inapaswa kuwekeza kwenye afya ya akili kwa kiasi kikubwa zaidi. Uwekezaji katika afya ya akili haulengi tu katika kutibu wale wenye mahitaji, lakini unalenga katika kuimarisha afya ikiwamo udhibiti kwenye matumizi ya vilevi kama pombe na sigara, kufanya mazoezi, lishe bora na kuimarisha uhusiano kwenye jamii,” amesema Dk Ubuguyu.





Download our APP from Google Playstore using the link here>>>

Join Our Telegram Channel for Daily Updates CLICK HERE

No comments:

Post a Comment

Edusportstz