Waziri Jafo atoa angalizo kumbi za starehe nchini - EDUSPORTSTZ

Latest

Waziri Jafo atoa angalizo kumbi za starehe nchini





SERIKALI imewataka wamiliki wa nyumba za ibada na kumbi za starehe wahakikishe sauti zitokanazo na shughuli zao hazizidi viwango vinavyokubalika kwa mujibu wa sheria huku ikiwaomba viongozi wa dini kupitia kamati za amani  kujadili namna bora ya kudhibiti kelele na mitetemo katika nyumba za ibada kwa lengo la kulinda afya za waumini wao.

Imesema itaanza kuchukua hatua kali za kisheria ikiwemo kifungo cha miezi sita gerezani kwa wamiliki wa makazi, viwanda na kumbi za starehe ambao maeneo yao yamekithiri kwa kelele na mitetemo.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali  leo June 29,2021,wakati akitoa taarifa kuhusu mkakati wa serikali katika kudhibiti kelele na mitetemo inayoathiri mazingira kwa jamii. Waziri wa Nchi,Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira,Seleman Jafo amesema kiwango cha sauti katika maeneo ya makazi   ni usiku  35 na mchana 50.

Mkutano huo pia ulihudhuriwa na Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto,Dk.Doroth Gwajima,Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Khamis Chilo,Naibu Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia,Omari Kipanga,Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi,Angelina Mabula,Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu,Walemavu,Ummy Ndairenanga na Naibu Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo,Paulina Gekul.


 
Waziri huyo amesema watakaobainika kukiuka Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004 inayokata kelele zilizopitiliza, watakabiliwa na adhabu ya kifungo cha miezi sita gerezani, au kulipa faini ya sh. milioni moja.  

“Katika siku za hivi karibuni kumekuwepo ongezeko kubwa la kero zitokanazo na kelele na mitetemo katika maeneo mbalimbali nchini,” amesema.

Amesema katika kipindi cha mwaka 2021/2020, Mamlaka ya Udhibiti na Uhifadhi wa Mazingira (NEMC) ilipokea jumla ya malalamiko 165 kutoka Dar es Salaam, Dodoma, Arusha, Mbeya, Mwanza, Morogoro na Tabora.

Waziri Jafo amesema katika kipindi cha Januari mpaka Machi mwaka huu, NEMC, ilipokea malalamiko 93 kutoka kanda mbalimbali ambapo Kanda ya Kati ilipokea malalamiko 30, Kanda ya Kaskazini (12), Kanda ya Ziwa (21), Kanda ya Nyanda za Juu Kusini (6) na malalamiko 31 kutoka Kanda ya Mashariki.

“Serikali imedhamiria kulinda afya za wananchi wake kwa sababu kelele na mitetemo imekuwa ikisababisha madhara ya kiafya kwa binaadamu kama kupoteza usikivu, kuondoa utulivu, kupunguza ufanisi wa kazi na kuzuia watu wasipate usingizi,athari za kisaikolojia kwa watoto, magonjwa ya moyo, usumbufu kwa wagonjwa, kupunguza umakini wakati wa kujisomea na kuleta kero kwa jamii.”amesema.

Katika kudhibiti hali hiyo, Waziri huyo ametoa  maagizo kwa kila mwananchi ahakikishe shughuli anazozifanya hazisababishi kelele na mitetemo.

Pia, amewaagiza  wamiliki wa nyumba za ibada na kumbi za starehe wahakikishe sauti zitokanazo na shughuli zao hazizidi viwango vinavyokubalika kwa mujibu wa sheria.


 
“Wamiliki wa maeneo ya burudani na starehe wazingatie matumizi ya vipima kelele na vizuia sauti kama ilivyoelekezwa katika leseni zao. Pia, wananchi wahakikishe ajenda ya kelele na mitetemo katika mikutani yao,” amesema

Aliwaomba viongozi wa dini kupitia kamati za amani kujadiliana kwa pamoja kupata njia bora ya kudhibiti kelele katika nyumba zao za ibada.



Kwa upande wake,Waziri wa Afya, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Gwajima, amesema kelele na mitetemo zimekuwa zikisababisha madhara mbalimbali kiafya.

Amesema kelele zinasababisha uchovu wa akili, msongo wa mawazo unaosababishwa na kutokulala kwa sababu ya kelele na hatimae kusababisha presha.

“Ndio maana siku hizi kuna ongezeko kubwa ya presha kwa watoto, mtoto anashindwa kupumzika kwa sababu ya kelele na ndio maana usiku utakuta mtoto nashtuka mara kwa mara,”amesema.




Download our APP from Google Playstore using the link here>>>

Join Our Telegram Channel for Daily Updates CLICK HERE

No comments:

Post a Comment

Edusportstz