Wagombea 74 wa uchaguzi wa TFF waingiza Sh 18.4 milioni katika shirikisho hilo - EDUSPORTSTZ

Latest

Wagombea 74 wa uchaguzi wa TFF waingiza Sh 18.4 milioni katika shirikisho hilo



Kwa mujibu wa taarifa kutoka TFF mgombea urais anapaswa kulipia 500,000, mgombea nafasi ya makamu wa rais gharama ya kuchukua fomu ilikuwa 300,000 na wajumbe waliochukua fomu za kuwania ujumbe wa kanda mbalimbali wamelipa 200,000 kila mmoja.
By Fredrick Nwaka, Mwananchi fnwaka@mwananchi.co.tz


Dar es Salaam. Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limevuna Sh. 18.4 Milioni kutola kwa wagombea 74 waliochukua fomu za kuwania nafasi mbalimbali kwenye uchaguzi ujao.


Kwa mujibu wa taarifa kutoka TFF mgombea urais anapaswa kulipia 500,000, mgombea nafasi ya makamu wa rais gharama ya kuchukua fomu ilikuwa 300,000 na wajumbe waliochukua fomu za kuwania ujumbe wa kanda mbalimbali wamelipa 200,000 kila mmoja.


Wagombea 10 wa nafasi ya urais wameiingizia TFF Sh 5 milioni, nafasi ya makamu wa rais inawaniwa na watu sita (6) wameiingizia TFF Sh.1.8 milioni wakati wanaowania ujumbe wa kamati ya utendaji kupitia kanda 13 za kisoka wapo 58 wameiingizia TFF, Sh.11.6 milioni.


Mchakato wa kuchukua fomu umekamilika leo saa 10 jioni na kesho kamati ya uchaguzi inayoongozwa na wakili Revocatus Kuuli itaanza kupitia fomu za wagombea.


Akizungumza jijini Dar es Salaam Ofisa Habari wa TFF Alfred Lucas alisema kamati ya uchaguzi itaanza kupitia taarifa za wagombea mbalimbali kuanzia kesho Juni 21.


"Kamati ya wakili Revocatus Kuuli kuanzia Juni 21 hadi 23 itapitia majina ya wagombea kabla ya kupitisha orodha ha mwisho,"alisema Lucas.


Miongoni mwa wagombea waliojitokeza dakika za mwisho kuchukua na kurejesha fomu ni Emmanuel Kimbe anayewania nafasi ya urais, Jamhuri Kihwelo anayewania ujumbe kupitia kanda ya Dar es Salaam na Stephen Mwakibolwa anayewania nafasi ya makamu wa rais.


Lucas aliongeza kuwa wagombea wote waliochukua fomu wamerejesha wenyewe na wengine wamerejesha kwa kutumia wawakilishi wao.


Uchaguzi mkuu wa TFF umepangwa kufanyika Agosti 12 mkoani Dodoma.


Download our APP from Google Playstore using the link here>>>

Join Our Telegram Channel for Daily Updates CLICK HERE

No comments:

Post a Comment

Edusportstz