Ifike Mahali Wema Umuamkie Mobeto - EDUSPORTSTZ

Latest

Ifike Mahali Wema Umuamkie Mobeto

 


KUTANGULIA sio kufika! Ndio unavyoweza kusema. Mrembo wa taifa, Tanzania Sweetheart Wema Sepetu alitangulia kuchomoka kwenye umaarufu lakini mwanamitindo Hamisa Mobeto akaja baadaye na sasa anaonekana kabisa anakwenda kumfunika dada yake huyo.

Iko hivi, tunapozungumzia mafanikio ya umaarufu siku zote tungaangalia dili ambazo msanii husika anakula na kuweza kumuingizia kipato cha kutosha kwenye akaunti yake.

Umaarufu wenye faida. Sio unakuwa maarufu tu halafu mfukoni unakuwa hana kitu sasa hiyo ina maana gani? Unakuwa maarufu lakini mtu akikuangalia unaishi mahali pazuri, unatembelea usafiri mzuri, una dili za matangazo makubwa ambayo yanakuingizia fedha.Kuweka rekodi sawa, Wema ni zao la Miss Tanzania mwaka 2006.

Huu mwaka ulizalisha mastaa wengi sana kwenye kipengele cha ulimbwende maana mastaa kama Irene Uwoya, Aunt Ezekiel, Jokate Mwegelo (sasa ni DC) na Lisa Jensen.

Wema alikuwa Wema kweli baada tu ya kushinda taji hilo na kuanza kuigiza. Akajizolea umaarufu mkubwa kwenye vyombo vya habari na hata kwenye mitandao ya kijamii pale iliposhika hatamu.

Wema alikuwa anapendwa kwa kila kitu. Kuanzia sauti yake hadi maisha yake ya kila siku. Drama za mahusiano yake hata zilikuwa haziwaboi sana mashabiki wake, waliendelea kumpenda na kumsapoti katika kila jambo lake.

Wema alikuwa na jeshi kamili ambalo likiamua kumvaa mtu huko mtandaoni lazima aipatepate. Kama ni kumuanika mambo yake watamchafua vya kutosha maana wapo wengi na silaha yao ni maneno na picha.

Tukimweka kando Wema, Mwaka 2010 ndio mwaka ambao Hamisa alikuja kwenye ulimwengu wa mastaa. Hapo ukipiga mahesabu ya miaka, Mobeto alikuja miaka minne baada ya Wema kuweka umalkia kwenye ulimwengu wa mastaa

Alitokea kwenye shindano la After School Bush lililokuwa linaandaliwa na vijana wa Clouds FM, aliweza kuonesha kipaji chake kwenye ulimwende baada ya kushinda kuwa Miss After School Bush 2010.

Mwaka 2011 Hamisa alishiriki mashindano ya Miss Dar Indian Ocean na alifanikiwa kushika nafasi ya pili, pia mwaka huohuo alikua mshindi wa pili wa Miss Kinondoni na kufanikiwa kuingia kwenye Nusu Fainali ya Miss Tanzania.

Mwaka 2012 Hamisa alishiriki kwenye mashindano ya Miss Univeristy Afrika na kuingia hatua ya 10 bora.Kutokea hapo, Hamisa amekuwa gumzo kwenye tasnia ya uanamitindo, filamu na Bongo Fleva. Hamisa ni video queen na wengi waliweza kumuona kwenye video ya Quick Rocka ya My Baby.

Mwaka 2014, Mobeto alitokea kwenye cover page la Pulse Magazine la nchini Kenya. Akiwa Ndio kwanza ana miaka 21. Sasa hivi ninapoandika makala haya, Mobeto yupo juu zaidi ya Wema kwa maana ya mafanikio.Mobeto anakula madili ya ubalozi kama hana akili nzuri.

Ametoka kufanya tangazo la kinywaji chenye jina kubwa duniani. Kinywaji kile kinatangazwa na mastaa wakubwa akiwemo Rick Ross na wengine kibao.Mobeto amejiongeza kwenye muziki, huko sasa hivi anaingiza pesa kupitia mtandao wa YouTube.

Mobeto anapiga madili ya ubalozi yenye maana, Wema anatangaza matangazo ya waganga.

Kwenye upande wa nyumba, yawezekana Mobeto hajajenga lakini anakaa kwenye nyumba nzuri kuliko ya Wema. Usisahau hata usafiri, Mobeto anatumia usafiri mzuri na sina hakika kama Wema kwa sasa anamiliki gari lake mwenyewe.

Ni dhahiri kwa upepo ulivyogeuka, kwa sasa Wema anapaswa kujifunza kupitia kwa Mobeto maana mwenzake amejua kuzitumia fursa.

Achana na starehe ambazo kila mtu anafanya lakini kuna kila sababu ya kuweka kiba au kuwekeza kwenye mambo ya maendeleo.Angalia, Mobeto anayo biashara ya duka ambalo Wema lilimshinda kuendesha.

Wema ajifunze nini shida? Ni marafiki au ni kitu gani kinamkwamisha? Akipata majibu basi ajiongeze kwani mtaji wa watu anao. Apambane na anaweza siku moja kusimama tena





Download our APP from Google Playstore using the link here>>>

Join Our Telegram Channel for Daily Updates CLICK HERE

No comments:

Post a Comment

Edusportstz