WOSIA WA MAMA KWA BINTI YAKE KUHUSU MAISHA NDANI YA NDOA - EDUSPORTSTZ

Latest

WOSIA WA MAMA KWA BINTI YAKE KUHUSU MAISHA NDANI YA NDOA

Image may contain: 2 people, people smiling


"Mwanangu ndoto yako ya kuolewa imetimia ila ndoto yako ya kuwa na familia bora ndio inaanza rasmi yakupasa kutambua sasa umeingia ulimwengu mpya na sayari mpya inayohitaji uvumilivu, ukakamavu, heshima, nidhamu, ibada na maombi ya hali ya juu ili uweze kuishi kwa amani na furaha. Wapaswa kuwatambua WANAUME hakika upendo na mahaba aliyokuwa akikuonyesha mmeo kipindi chenu cha uchumba ni ngumu mno kubaki vile vile mpaka ndani ya ndoa.

Wanaume ni kama vinyonga, huja kukutega na kukunasa kwa rangi uipendayo ila wakishakupata hukuonyesha rangi zao asili, simaanishi kuwa ni WAONGO AU WABAYA la hasha ila kama maua wamejaliwa nakshi na utashi wa pekee kuwapata wawapendao hivyo mnapokua ndani ya ndoa ndipo uhalisia wao huibuka na kuanza kukuzuia na kukukataza yale waliyokua wakikunyamazia kipindi cha uchumba ili kukuridhisha ukubali wakupate. Vaa vazi la fikra mpya mwanangu, ndoa yahitaji mawazo na mtazamo mpya kuhusu maisha, sahau kuhusu out za ovyo, night clubs, disco, beach, mitindo na anasa zingine anza kuwaza kuhusu namna ya kuboresha ndoa na familia yako, waza kuhusu mmeo na watoto wako, mshauri mmeo kuhusu maendeleo na miradi yenu, punguza mizaha na ikibidi kata kabisa mawasiliano na marafiki zako wa zamani waliozoea utani na wewe wasijekukuvunjia ndoa.
Siku zote hakikisha unakua faraja kuu kwa mmeo na chanzo kikuu cha furaha na amani yake epuka kuwa mzigo na kero kwa mmeo, MTII MMEO ishi nae katika namna ambayo anapendelea zaidi mkewe uwe, anapokata tamaa na kulemewa changamoto za kikazi na maisha mtie moyo, mfariji mpe tabasamu na busu shavuni mwambie, "USIKATE TAMAA MME WANGU, MUNGU NI MWEMA HAKIKA TUTASHINDA" hapo mmeo siku zote hata akiwa kazini au safarini mbali atakua akikumiss na kukuwaza wewe, akili yake itakua umeiteka hatokaa akuchoke wala kutafuta michepuko maana wewe ndie faraja kuu ya moyo wake.

Ndani ya ndoa kuna changamoto zake tena kali mno ila kwa kuwa umeshakubali kuingia basi huna budi kuzihimili, ushauri na mawazo ya marafiki zako kamwe yasije kukutoa kwenye mstari ukashindwana na mmeo, angalia watu wa kuwaomba ushauri usijevunjiwa ndoa na mashangingi waliozoea kuachika, ikitokea mmekosana tumia hekima, ushauri wa wazee na busara za wazazi usiwe mtu wa kiburi, shari, mbishi na jeuri, ndoa itadumu.

Sina mengi mwanangu zaidi sana usiache kusali na kumuomba Mungu ailinde ndoa yenu dhidi ya hila zote zitakazolengwa kuwaangusha, Mungu awabariki mpandapo na mvunapo, awazungushie ulinzi wa malaika wake katika kila mnalolipanga na kulifanya na mmeo mfanikiwe. Awape watoto wazuri wataokua baraka na neema katika familia yenu, mtukumbuke pia wazazi wenu hakika furaha na amani katika ndoa yenu itakua ni faraja yetu kuu uzee wetu wote hadi kifo".


Nakutakia siku Njema Mungu Akubariki na kukulinda




Download our APP from Google Playstore using the link here>>>

Join Our Telegram Channel for Daily Updates CLICK HERE

No comments:

Post a Comment

Edusportstz