Yanga kucheza na Geita Gold - EDUSPORTSTZ

Latest

Yanga kucheza na Geita Gold


YANGA SC leo inatarajiwa kucheza mchezo wa kirafiki na timu ya Geita Gold Uwanja wa shule ya Msingi Waja, Geita.

Yanga imewasili Geita leo ikitokea Mwanza ambako jana ilivuliwa ubingwa wa Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), michuano inayojulikana kama Azam Sports Federation Cup (ASFC) kufuatia kipigo cha 1-0 kutoka kwa Mbao FC katika mchezo wa Nusu Fainali Uwanja wa CCM Kirumba.

Ikumbukwe Yanga iliweka kambi ya siku mbili Geite ikitokea Dar es Salaam kujiandaa na mchezo dhidi ya Mbao FC na ulikuwa ni mpango ipite hapo kwa mchezo mmoja wa kirafiki kulipa fadhila.

Na mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara wanatarajiwa kuondoka Geita Alhamisi kwenda Mwanza kuunganisha ndege kurejea Dar es Salaam.

Yanga SC inatarajiwa kushuka tena dimbani Mei 6 kumenyana na Tanzania Prisons katika mchezo wa kiporo wa Ligi Kuu.

Kikosi kizima cha Yanga kipo Mwanza isipokuwa mabeki Mtogo Vincent Bossou na Pato Ngonyani na washambuliaji Mzimbabwe Donald Ngoma na Malimi Busungu. Bossou na Ngoma ni majeruhi wakati Busungu na Ngonyani wana matatizo ya kifamilia.

Mapema mwanzoni mwa msimu, Yanga ilivuliwa taji la Ngao ya Jamii baada ya kufungwa na Azam FC kwa penalti 4-1 kufuatia sare ya 1-1 katika mchezo wa kuashiria ufunguzi wa msimu mpya, Agosti 17, mwaka jana.

Na sasa Yanga ina jukumu la kutetea taji lake moja lililobaki na kubwa zaidi, la Ligi Kuu ambako wanakabana koo na wapinzani wao wa jadi, Simba SC.

Simba wapo kileleni mwa Ligi Kuu kwa pointi zao 59 za mechi 27, wakifuatiwa na Yanga SC wenye pointi 56 za mechi 25.


Download our APP from Google Playstore using the link here>>>

Join Our Telegram Channel for Daily Updates CLICK HERE

No comments:

Post a Comment

Edusportstz